Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba SC Salim Abdallah ‘Try Again’ amewaambia Mashabiki na Wanachama kuwa wajiandae kufurahia msimu ujao kwa kuanzia ‘Simba Day’ huku akitamba kutangaza ubingwa wa Ligi Kuu Bara wakiwa wamebakisha michezo mitano mkononi.

Kauli hiyo ameitoa wakati wakiwa katika maandalizi ya Tamasha la Simba Day litakalofanyika Jumapili (Agosti 06) kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.

Katika tamasha hilo, Simba SC inatarajiwa kucheza mchezo maalum wa kirafiki dhidi ya Power Dynamos ya nchini Zambia sambamba na utambulisho wa wachezaji wake wapya na benchi la ufundi.

Akizungumza jijini Dar es salaam Abdallah amesema kuwa: “Kwa usajili huu ambao Simba SC tumeufanya, basi naamini msimu ujao tutabeba ubingwa wa Ligi Kuu Bara kabla ya mechi tano za mwisho, yaani tukiwa na mechi tano mkononi.

“Usajili wetu tuliofanya umeendana na mahitaji na mapendekezo ya kocha ambayo ameyafanya kwa kuwasajili wachezaji aliowahitaji.

“Hivyo mashabiki wa Simba SC wajiandae kufurahi msimu ujao, kwa kuanzia siku ya Simba Day Jumapili hii na kuendelea hadi katika Ngao ya Jamii.”

Rais Samia aungwa mkono uwezeshaji Vijana, Kinamama
DCEA, JKT Ruvu wateketeza mashamba ya Bangi