Mjadala mkubwa umetokea Bungeni mjini Dodoma mapema hii leo mara baada ya wabunge wa viti maalumu kuhoji uhalali wa kutokuwepo kwenye mgawo wa fedha za mfuko wa jimbo.

Mjadala huo umeibuka mara baada ya Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, Suleiman Jafo kusema kuwa fedha hizo haziwahusu wabunge hao hali ambayo imeibua maswali mengi kwa wabunge hao.

Akijibu hoja hiyo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, George Simbachawene  kuhusu mgawo wa fedha za mfuko wa Jimbo, amesema kuwa mfuko huo upo kwa ajili ya majimbo na si kuwalipa wabunge wa viti maalumu.

Amesema kuwa yeye yupo kwa ajili ya kusimamia mfuko huo uliopo kwa mujibu wa sheria za bunge hivyo hana nanma ya kubadilisha sheria hiyo ili kuwawezesha wabunge hao kupata fedha hizo.

Aidha, Katika hatua nyingine, Simbachawene ameongeza kuwa kwa upande wa Zanzibar kuhusu fedha hizo amesema kuwa atawasiliana na Ofisi ya Makamu wa Rais ili kuweza kuweka utaratibu maalum wa kuharakisha upatikanaji wa fedha hizo.

“Mfuko huu hauwahusu wabunge wa viti maalum, napata wakati mgumu kama Jimbo moja linakuwa na idadi kubwa ya wabunge wa viti maalum, ina maana fedha hizi zitaishia kwenye mgawo wa wabunge,”amesema Simbachawene.

Kamil Grosicki Awabwaga Roberto Firmino, Eden Hazard
?LIVE: Yanayojiri Bungeni Dodoma leo Mei 5, 2017