Licha ya kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Mashujaa FC jana Alhamis (Februari 08) katika Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es salaam, Kocha Mkuu wa Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Young Africans Miguel Angel Gamondi amesema ameanza kufanyia kazi safu yake ya ulinzi na kiungo ili kuwa na mwendo bora katika kila mechi.

Gamondi ameweka wazi kuwa safu yake ya ulinzi inatakiwa kuwa makini na kuwa na utulivu wanapokuwa wanashambuliwa.

Amesema kwa sasa ligi kuu imekuwa ngumu kutokana na kila timu kuhitaji ushindi hivyo lazima wawe makini katika kila mchezo ambapo ameweka lengo la kwanza ni kupata pointi tatu na kutoruhusu kufungwa.

“Kwa sasa hatutakiwa kuruhusu mabao golini kwetu, ndio nafahamu tumekuwa na tatizo dogo kwenye kufunga lakini naamini ni tatizo la muda mfupi tu, katika mbio za ubingwa hapa tulipofikia tunapaswa kutoruhusu kufungwa alafu tupiganie pointi tatu.” amesema Gamondi.

Gamondi amesema ni muhimu kwa wachezaji wote kucheza kwa ushirikiano kwenye kutimiza majukumu yao ikiwa ni kuzuia kufungwa na kufunga mabao kwenye mechi zao.

Amesema wana kazi kubwa ya kufanya kwenye kila idara kuanzia ile ya ulinzi ambayo ni muhimu kuhakikisha hawafungwi na hiyo itawapa nguvu kutafufa mabao mengi ya kushinda.

“Ni rahisi kuwa na mwendo mzuri pale unapokuwa na timu ambayo haifungwi lakini ikitokea mkifungwa, presha inakuwa kubwa kwenye kutafuta mabao na kupata ushindi,” amesema Gamondi.

Amesema anaimani na wachezaji wake na anajua wanapambana kuhakikisha timu inafanya vizuri na kufikia malengo yao.

Young Africans inaongoza ligi ikiwa na pointi 37 ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 31 huku Simba SC ambao wapo nyuma kwa mchezo mmoja inashika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 29.

Watendaji Kata waaswa kusimamia ulinzi, usalama Vijijini
Ondokeni mabondeni kupunguza maafa - Majaliwa