Uongozi wa Simba SC leo Jumatano (Juni 21) ulitarajiwa kumshusha beki wa mpya wa kati, Che Fondoh Malone kutoka nchini Cameroon tayari kumalizana naye kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara pamoja na michuano ya kimataifa.

Malone ambaye ni beki wa Coton Sports ya kwao Cameroon, inaelezwa amekubali kujiunga na Simba SC kwa mkataba wa miaka miwili na anachukua nafasi ya Joash Onyango.

Simba SC wamekuwa wakipambana kuhakikisha wanaijenga upya timu yao kufuatia kufanya vibaya msimu uliopo kwa kushindwa kushinda Kombe lolote la kimashindano ambapo kwenye Ligi Kuu Bara wamemaliza katika nafasi ya pili nyuma ya Mabingwa Young Africans wakati kwenye Kombe la FA wakiishia nusu fainali huku Ligi ya Mabingwa wakimaliza kwenye Robo Fainali.

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya bodi ya timu hiyo zinaeleza kuwa beki huyo alitarajiwa kutua usiku wa kuamkia leo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere akitokea kwao Cameroon akipitia nchini Ethiopia.

Chanzo hicho kimendelea kusema kuwa, beki anakuja kwa ajili ya kukamilisha vipengele vilivyobakia kabla ya kusaini mkataba na timu hiyo ambao unatajwa kuwa ni wa miaka miwili.

“Ni kweli Malone aliatarajiwa kuwasili Tanzania leo Jumatano, anakuja kwa lengo moja tu kukamilisha taratibu za kusaini kwa kuwa mambo yote yalishamalizwa.

“Anatokea Cameroon lakini atatumia usafiri wa Ethiopian Airlines hivyo hapa ataingia usiku mkubwa, na unajua namna viongozi wanavyopambana kuhakikisha wanajenga timu kubwa ya ushindani kuelekea msimu ujao,” amesema mtoa taarifa.

Lakini kwa upande wa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’, alishaweka wazi juu ya suala la kuboresha benchi la ufundi la timu hiyo kwa kusema kuwa wanayajua makosa waliofanya msimu huu hivyo wamejipanga kufanya maboresho makubwa katika benchi la ufundi la timu hiyo ili kuweza kufanya vizuri msimu ujao.

Simba SC: Hatutakosea usajili 2023/24
RS Berkane yakataa kumuuza Adebayor