Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan amefanya ziara nchini Saudi Arabia kwa nia ya kutafuta ufumbuzi wa mvutano baina ya Qatar na nchi nne za kiarabu, ambazo ni Saudi Arabia, Bahrain, Umoja wa Falme za kiarabu na Misri.

Rais Erdogan amesema kuwa hakuna mtu yoyote anayepata faida kwa kuendeleza mgogoro huo, hivyo katika ziara yake hiyo ataanza kukutana na uongozi wa Saudi Arabia mjini Jeddah kabla ya kuelekea Kuwait nchi ambayo ni mpatanishi katika mgogoro huo na baadaye kuelekea Qatar.

Aidha, akiwa katika uwanja wa ndege wa Istanbul nchini Uturuki kabla ya kuanza safari yake, Rais Erdogan amewatuhumu maadui kwamba wanataka kuuchochea zaidi mvutano huo na kuzusha hali ya wasiwasi baina ya ndugu katika ukanda huo.

Hata hivyo, Rais huyo ameisifu Qatar kwa kuonyesha msimamo wake katika mgogoro huo huku akisema ni nchi iliyoamua kufuata njia ya mazungumzo kuupatia ufumbuzi mgogoro huo na kuwa Uturuki ina matumaini kwamba ziara hiyo itasaidia kuleta mafanikio katika ukanda huo.

Mvutano baina ya nchi hizo za Ghuba ulianza tarehe 5 mwezi Juni ambapo Saudi Arabia, Bahrain, Umoja wa Falme za kiarabu na Misri ziliamua kukata uhusiano wao na Qatar kwa kuituhumu nchi hiyo kwamba inawaunga mkono watu wenye itikadi kali na kwamba inashirikiana kwa karibu zaidi na Iran taifa ambalo ni la kishia

Kafulila afunguka mazito baada ya JPM kumshukuru kwa kuibua sakata la IPTL
Video: JPM amshukia aliyemuita Kafulila 'Tumbili' Escrow, Jinsi walivyotiwa mbaroni kwa 'unga'