Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kuhakikisha wanakagua vifaa vyote vya kujikinga na corona vinavyoingia nchini.

Akizungumza na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama, leo, Aprili 22, 2020, Rais Magufuli amesema kuwa katika nchi nyingine wametilia shaka baadhi ya misaada ikiwa ni pamoja na barakoa.

“Kuna nchi baadhi wameanza hata kuuliza hivi vifaa vya misaada ambavyo vinatumika. Na ndio maana nimeona nizungumze hili kwa vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na Wizara ya Afya waanze kushughulikia hata vitu tunavyopewa kama zawadi ili visije vikatuletea madhara,” amesema Rais Magufuli.

“Unapoletewa mask ya kujikinga puani (barakoa) ni lazima tujue hiyo mask aliyeitengeneza, aliyei-supply na misingi ya kutuletea; kwa sababu la sivyo tunaweza tukajikuta tunaambukizwa corona kwa mask za kutoka nje,” ameongeza.

Rais ametoa wito kwa taasisi na viwanda nchini kuanza kutengeneza barakoa huku akiwapongeza Watanzania ambao wamechukua hatua ya kuanza kushona wenyewe barakoa.

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli alishangaa utaratibu ulikuwa umeanza kuwekwa na Wizara wa kupuliza dawa ‘fumigation’ kwenye vyombo vya usafiri.

“Wizara ya Afya nimeambiwa siku za nyuma walitoa amri ya kufanya furmigation… mabasi yaende wapi yanafanyiwa fumigation, yakifika sokoni yanafanyiwa fumigation. Na hili Dar es Salaam nililiona sana na Mwanza, hakuna fumigation yoyote inayoweza kuua corona, na hili Watanzania ni lazima tuambizane ukweli,” amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli alisema kuwa kama fumigation ingeweza kuua virusi vya corona, basi nchi zinazoendelea wangehakikisha wanamwaga kwenye maeneo yao yote kwakuwa wana uwezo huo.

Magufuli: Tutumie njia asili kupambana na Corona
Live: Magufuli Chato: "Dar es salaam haitafungwa"