Korea Kaskazini imeendelea na mpango wake wa majaribio ya silaha nzito ambapo jana usiku imeripotiwa kufyatua kombora lingine zito kutoka Magharibi mwa eneo lake.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na maafisa wa Japan na Korea Kaskazini, kombora hilo lilifyatuliwa majira ya saa tatu na dakika arobaini usiku kwa saa za eneo hilo, na lilitua katika eneo muhimu la kiuchumi la bahari nchini Japan.

Shirika la habari la Yonhap limekariri tamko la jeshi la Japan kuwa kombora lililofyatuliwa lilisafiri umbali wa kilometa 930 na lilichukua dakika 40 kabla ya kutua, kitendo kilichozua taharuki.

Hili ni jaribio la 11 la makombora ya Korea Kaskazini kwa mwaka huu, ingawa majaribio ya hivi karibuni yanaonekana kufanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Jaribio la mwisho lilikuwa mwezi Mei mwaka huu, katika maeneo mawili tofauti ambayo yote yalielekezwa baharini nchini Japan.

Katibu Mkuu wa Baraza la Mawazili la Japan, Yoshihide Suga ameeleza kuwa uchokozi unaofanywa na Korea Kaskazini hauvumiliki. Ameongeza kuwa taifa hilo linalaani kwa nguvu zote vitendo hivyo na hatua stahiki zitachukuliwa.

Naye Rais wa Korea Kusini, Moon Jae ametoa wito wa kufanyika kwa kikao cha dharura cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kujadili hatua za Korea Kaskazini, wito aliousisitiza pia wakati wa kikao chake na Rais wa Marekani, Donald Trump ndani ya Ikulu ya Marekani.

Rais Trump pia aliendelea na mfululizo wa maonyo kwa Korea Kaskazini, akisema kuwa uvumilivu umefika kikomo na sasa ‘inatosha’.

Magazeti ya Tanzania leo Julai 4, 2017
Video: Jamal Malinzi na wenzake waendelea kusota rumande