Mshauri Mkuu wa Rais Donald Trump, amejiuzulu baada ya kukabiliwa na kashfa ya udanganyifu, kuhusu mazungumzo aliyoyafanya na balozi wa Urusi,

Ikulu ya White House teyari imeshamtangaza atakae chukua nafasi yake na imefanya hivyo mara baada tu ya uamuzi wake wa kujiuzulu.

Mshauri huyo, Michael Flynn hapo mwanzoni alikanusha kuhusisha suala la vikwazo dhidi ya Urusi, katika mazungumzo na balozi wa Urusi nchini Marekani Sergei Kislyak, wakati ambapo alikuwa hajaanza rasmi majukumu yake.

Aidha, hii linachukuliwakama pigo kubwa kwa utawala wa Donald Trump ambao haujamaliza hata  mwezi mmoja. Kwa siku kadhaa uvumi umekuwa ukienea, kwamba Flynn ambaye ni Jenerali mstaafu, alimdanganya Makamu Rais Mike Pence, ambaye alijitokeza hadharani kumtetea.

Katika barua yake ya kujiuzulu, Flynn amesema ”bila kukusudia” alimpa Makamu Rais ”taarifa ambazo sio kamilifu” kuhusu mazungumzo yake ya simu na balozi  Kislyak wa Urusi.

Hata hivyo, Ikulu ya White House mjini Washington imesema kuwa imemteuwa Luteni Jenerali Joseph Kellogg ambaye alikuwa mwenyekiti wa baraza la majenerali, kukaimu katika nafasi iliyoachwa wazi na Michael Flynn.

Vyombo vya habari nchini Marekani viliripoti jana Jumatatu, kwamba utawala wa Donald Trump ulikwishatahadharishwa mapema mwaka huu kuhusu mahusiano kati ya Michael Flynn na Urusi.

Marekani yasema Korea ya Kaskazini ni tatizo
Marco Verratti, Gerard Pique Kurejea Dimbani Leo