Shirikisho la Soka nchini (TFF) sasa linaonekana halitakuwa na utani linapofikia suala la bima kwa wachezaji.

Mara kadhaa, suala hilo la bima limekwua likisisitizwa lakini bila ya mafanikio na klabu huona ni kama mzaha fulani hivi.

Rais wa Shirikisho la Soka nchini, Wallace Karia amesema kamwe hataruhusu klabu yoyote kucheza Ligi Kuu Bara kama itakuwa haijawakatia bima wachezaji wake.

Karia amesema hilo litaanza kwa msimu ujao wa 2018/2019 na hakutakuwa na msamaha.

Ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa semina ya utawala bora kwa klabu za ligi kuu na Ligi Daraja la Kwanza iliyofanyika jana Rombo Green View iliyokuwepo Ubungo jijini Dar es Salaam ambayo ilihusisha klabu kongwe za Simba na Yanga.

Semina hiyo, iliandaliwa na Kampuni ya Maendeleo na Utafiti wa Michezo (ISDI) kwa kushirikiana na Alliance Life Assuarance na TFF kwa lengo la kutoa elimu kwa viongozi wa klabu kujua jinsi ya utawala, kujiongoza na kutafuta wadhamini.

Akizungumza na Waandishi wa Habari kabla ya kufungua semina hiyo, Karia alisema kikubwa anataka kuona klabu maendeleo na mafanikio kwa klabu hizo huku akiamini kupitia semina hiyo wawakirishi hao watapata elimu nzuri.

“Hakutakuwa na utani juu la hili la bima ni lazima kila klabu iwakatie bima ya afya wachezaji wake na uzuri wapo hapa Alliance Life Assuarance ambao wanausika na bima.

“Kama klabu haitakuwa imewakatia bima wachezaji wake, basi haitacheza ligi kuu msimu ujao na hilo nitahakikisha ninalisimamia vizuri na kama itakuwepo klabu imeshindwa kutimiza hilo basi itatakiwa kuwasiliana na bodi ya ligi tujue jinsi ya kuwasaidia ili wakatiwe bima,” alisema Karia.

Athuman Bilal: Simba ni timu ya kawaida
Mashambulizi yaendelea nchini Syria