Waziri wa Elimu, Profesa. Joyce Ndalichako amesema kuwa  serikali itagharamia shughuli za mazishi ya Mwanafunzi  wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina ambaye ameuawa kwa kupigwa risasi Februari 16, 2018 eneo la Mkwajuni DSM.

Waziri Ndalichako amesema kuwa viongozi mbalimbali wameguswa na kifo hicho kwani mwanafunzi huyo hakuwa na hatia yoyote na kusema kifo chake ni pigo kubwa kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Mimi Waziri mwenye dhamani ya elimu nimesikitika sana kuona binti huyo amepoteza maisha akiwa katika kutekeleza shughuli zake za kielimu, Wizara yangu itagharamia mazishi ya marehemu Akwilina hadi hapo atakapopumzishwa katika makao yake ya milele, namuagiza Katibu wangu kuhakikisha kwa pamoja tunasimamia shughuli zote za msiba huu,”amesema Waziri Ndalichako

Aidha, Ndalichako amesema kuwa kifo cha mwanafunzi huyo kimetokea wakati akiwa kwenye harakati ya kupeleka barua ya maombi ya mafunzo kwa vitendo ambayo alikuwa akitegemewa kuanza Februari 26, 2018 na kudai kifo hicho kimezima ndoto yake na serikali kukipokea kwa masikitiko.

Hata hivyo, Waziri ameviomba vyombo vya usalama kufanya uchunguzi kwa haraka ili kuwatambua na kuwakamata watu ambao wamesababisha kifo cha mwanafunzi huyo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.

Chadema wataka Polepole ahojiwe
Video: Mbowe asakwa kuhusu kifo cha mwanafunzi