Kituo cha Sheria na haki za Binadamu (LHRC) kimeeleza kulaani vikali vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu vinavyoendelea nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa kituo hicho, Anna Mahenga amesema, pia wanalaani kitendo cha Wakala wa barabara nchini (Tanroads) kuidharau mahakama.

Amesema wameshangazwa na uamuzi wa Tanroads wa kubomoa nyumba za wananchi wa Kimara hadi Kiluvya wakati wanapingamizi la Mahakama.

“Tunalaani kitendo hiki na tunaona ilichofanya Tanroads ni kuidharau Mahakama ambapo kwa lugha ya kisheria tunaita Contempt of Court(kuiingilia Mahakama) “amesema

Mkurugenzi huyo pia amesema wanalaani kitendo cha kukamatwa ovyo kwa wanasiasa na kusema kitendo hicho ni kuminywa kwa haki za kisiasa.

“Hali hii imejitokeza sana kwa kuwanyanyasa wabunge wa vyama vya upinzani bila kufuata misingi ya kisheria na haki za binadamu “amesema

Amesema ukamatwaji wa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na Mbunge wa Bunda mjini Ester Bulaya aliyekamatwa akiwa hotelini kwa tuhuma za kutaka kuhudhuria mkutano nje ya jimbo lake na kudai kuwa huo ni ukiukwaji wa haki na kunyimwa uhuru wa vyama vya upinzani kufanya kazi yake.

Ndoa Ya Man Utd Na Zlatan Yafungwa Upya
FC Barcelona Yawinda Watatu Ujerumani