Mabeki wa Simba SC, Mohamed Hussein ‘Zimbwe Jr’ na Shomari Kapombe, wanaongoza kwa kutoa pasi za mwisho zilizozaa mabao upande wa mabeki mpaka sasa ambapo zimebaki raundi mbili ili kukamilika kwa msimu wa Ligi Kuu Tanzania Bara, imeelezwa.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Bodi ya Ligi ya Tanzania, Kapombe na Zimbwe Jr, wote wameshatoa ‘assist’ sita mpaka sasa ambapo kama itakwenda hivi hadi mwisho wataweka rekodi ya kuwa mabeki walioongoza kutoa pasi za mwisho katika Ligi Kuu Bara msimu huu wa 2022/23.

Wakati Kapombe akiwa ni beki wa kulia na kutegemewa wa Simba, Zimbwe ni beki wa kushoto na kutumainiwa na timu hiyo iliyoondolewa katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika hivi karibuni.

Nafasi ya pili kwa mujibu wa takwimu hizo inashikiliwa na Nicholaus Gyan wa Singida Big Stars ambaye ana ‘assist’ tano mpaka sasa, Joyce Lomalisa wa Young Africans akikamata nafasi ya tatu na ‘assist’ zake nne, Amos Kadikilo wa Geita Gold na Djuma Shaaban wa Young Africans hawa wana ‘assist’ mbili kila mmoja.

Takwimu zingine zilizotolewa ni makipa waliocheza mechi nyingi bila kuruhusu lango kuguswa, ambapo kipa wa Young Africans, Djigui Diarra amekuwa kinara kutokana na kuwa na ‘clean sheets’ 16 mpaka sasa. Hakuna kipa yoyote anayemfikia, hivyo tayari ameshakuwa mshindi kwa msimu huu.

Aishi Manula wa Simba anafuatia kwa kuwa na ‘clean sheets’ 12, Ali Ahmada wa Azam FC akiwa nazo nane, Metacha Mnata, ambaye amezichezea Singida Big Stars na Young Africans ana ‘clean sheets’ saba, huku makipa Benjamin Haule, Mahmoud Mroivil wa Coastal Union, Fikirini Bakari wa Ihefu na Said Kipao wa Kagera Sugar wenye ‘clean sheets’ sita kila mmoja.

Mshambuliaji wa Young Africans, Fiston Mayele akiwa na mabao 16 mpaka sasa anawaongoza kwa kupachika magoli huku kiungo mshambuliaji wa Simba, Clatous Chama, yeye anaongoza kwa ‘assist’ za jumla, akiwa ameshatoa pasi za mwisho 14 mpaka sasa, kiungo mwingine, Saido Ntibazonkiza, ambaye aliichezea Geita Gold na baadaye Simba, yeye amechangia mabao 22, ambayo ni mengi kwenye ligi kuliko mchezaji mwingine yoyote, akiwa amefunga mabao 10 na ‘asist’ 12.

Rais Mwinyi, Viongozi ACT-Wazalendo wakutana Ikulu
Uzinduzi wa Minara: Mtoto Georgina aketi katika kiti cha Rais