Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya kote nchini wahakikishe wanafikisha umeme kwenye vituo vya kutolea huduma za kijamii zikiwemo shule na hospitali.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na mamia ya wananchi na viongozi wa mikoa ya Lindi na Mtwara baada ya kuzindua kituo cha kuunganisha umeme wa gridi ya Taifa katika kijiji cha Mahumbika, wilaya ya Lindi mkoani Lindi.

“Wakati tukizindua miradi kama hii, niwasihi Wakurugenzi wa Halmashauri wahakikishe kuwa umeme unapelekwa kwenye taasisi za kutolea huduma zikiwemo shule zote za msingi na sekondari. Wakurugenzi tekelezeni hilo,” amesema Majaliwa.

Aidha, Majaliwa amesema malengo ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake ni kutaka Watanzania watumie umeme huo kukuza uchumi wao kupitia biashara za saluni, kuuza maji baridi au vinywaji baridi.

Hata hivyo, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na hadhara hiyo, Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amesema kuwa miezi mitatu iliyopita hapakuwa na nyaya wala nguzo za umeme kutoka Lindi kwenda Mtwara lakini mafundi wa TANESCO wamejitahidi na kuifanya kazi hiyo ndani ya muda mfupi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Erasto Zambi amesema kuwa tukio la uzinduzi wa mradi wa kuunganisha umeme wa gridi ya Taifa kwa mikoa ya Lindi na Mtwara ni la kihistoria.

Zimbabwe yawasilisha ombi rasmi kurejea Jumuiya ya Madola
Akamatwa na Polisi kwa kujifanya IGP Sirro