Mlinda mlango wa Newcastle Utd, Rob Elliot huenda akashindwa kucheza sehemu ya mwisho ya msimu huu, baada ya kuumia goti akiwa na timu yake ya taifa ya Jamuhuri ya Ireland.
Elliot alilazimika kutolewa uwanjani kwa machela, katika dakika ya 14 wakati wa mchezo wa kimataifa wa kirafiki kati ya Jamuhiri ya Ireland dhidi ya Slovenia uliochezwa usiku wa kuamkia hii leo.
Mlinda mlango wa klabu ya West Ham Utd, Darren Randolph alichukua nafasi ya Elliot ambaye alilazimika kukimbizwa hospitali kwa ajili ya kufanyia vipimo.
Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Jamuhuri ya Ireland, Martin O’Neill alithibitisha kuumia kwa mlinda mlango huyo mara baada ya mchezo kumalizika, kwa kusema Elliot alibainika kuwa na majeraha katika sehemu ya goti la mguu wake wa kulia.
Hata hivyo alidai kwamba jeraha hilo sio kubwa sana, japo hakufahamu kwa haraka kama anaweza kurejea uwanjani kwa haraka zaidi.
Kuumia kwa Elliot huenda ikawa mashaka makubwa kwa meneja mpya wa klabu ya Newcastle Utd, Rafael Benitez ambaye amepewa jukumu kubwa la kuhakikisha mambo yanakaa sawa hadi mwishoni mwa msimu huu, kwa kuibakisha The Magpies ligi kuu.
Elliot alionekana kuwa shujaa wakati wote akiwa langoni mwa Newcastle Utd, licha ya mambo kuwaendea mrama miezi kadhaa iliyopita, lakini uimara wake uliendelea kuwa tishio baada ya kuwasili kwa Benitez mwanzoni mwa mwezi huu.
Katika mchezo wa jana timu ya taifa ya Jamuhuri ya Ireland ililazimishwa matokeo ya sare ya mabao mawili kwa mawili.
Baadhi ya matokeo ya michezo mingine ya kimataifa ya kirafiki iliyochezwa usiku wa kuamkia hii leo.
Estonia 0-1 Serbia
Montenegro 0-0 Belarus
Georgia 1-1 Kazakhstan
Macedonia 0-2 Bulgaria
Ugiriki 2-3 Iceland
Gibraltar 0-5 Latvia
Norway 2-0 Finland
Luxembourg 0-2 Albania
Austria 1-2 Uturuki
Sweden 1-1 Jamuhuri Ya Czech
Uswiz 0-2 Bos-Herze
Ujerumani 4-1 Italia
Ureno 2-1 Ubelgiji
England 1-2 Uholanzi
Ufaransa 4-2 Urusi
Scotland 1-0 Denmark