Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed ameapishwa kuongoza kwa muhula wa pili, baada ya chama chake kushinda uchaguzi uliofanyika mwezi Juni mwaka huu.

Aidha Abiy ameapishwa kushika wadhifa huo huku Serikali yake ikiendelea kushutumiwa kutokana na hatua yake ya kuwafukuza kutoka nchini Ethiopia maafisa Saba wa mashirika ya kimataifa ya misaada ambao walikuwa wakitoa huduma katika jimbo la Tigray ambalo limeathirika kutokana na mapigano kati ya Wanajeshi wa Serikali na wapiganaji wa jimbo hilo.

Hata hivyo Ethiopia inatetea uamuzi wake kwa madai kwamba Maafisa hao wamekuwa wakiingilia mambo yake ya  ndani.

Kwa upande wake Umoja wa Mataifa umesisitiza kuwa Maafisa hao ambao ni wa kutoka Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF) na lile la kuratibu misaada ya Kibinadamu (UNOCHA)  wamekuwa wakitekeleza majukumu yao vema wakisaidia watu wanaokabiliwa na matatizo ikiwemo njaa na magonjwa.

Neema yawashukia waamuzi Tanzania
Gomes: Tumepata dawa ya kutetea ubingwa wetu