Mwanamuziki kutoka nchini Nigeria na mshindi wa tuzo ya Grammy, Burna Boy, amemwalika msanii wa Ghana Shatta Wale kuingia ulingoni wapigane ili kufikia muafaka wa mgogoro unaoendelea baina ya wasanii hao.

Wito huo wa Burna Boy umekuja kufuatia maneno makali aliyoyatoa msanii Shatta wale akiyaelekeza kwa wasanii wa nchini Nigeria akiwatolea malalamiko kuwa ni wabinafsi na wenye roho mbaya.

Burna amesema yuko radhi kuingia ulingoni kwa ajili ya kupigana na Shatta Wale ili amfundishe adabu kwa kile alichodai kuwa pambano hilo ndilo litakalokuwa suluhisho la migogoro inayoendelea na hata kama kuna matatizo mengine binafsi.

Mwimbaji huyo wa ‘Odogwu’ aliutumia ukurasa wake wa mtandao wa Instagram (Insta story)  yake kuyajibu maneno ya Shatta Wale aliyoyaandika kwenye mtandao wa Twitter Desemba 27.

Mengine aliyoyazungumza wakati akitumbuiza kwenye Freedom Concert huko nchini Ghana, ambapo aliwataja na kuwakashifu wasanii wote wa Nigeria kuwa hawana lolote na hata mtindo wao wa kuimba ni wa aina moja.

Burna boy ameamua kumpa Shatta Walle changamoto ya kupigana naye akisema “Ikiwa Shatta au mtu yeyote mwenye shida na mimi, bado niko tayari kupigana moja kwa moja”.

Shatta Wale pia ametilia mkazo suala la kuwazuia waghana kuwaunga mkono wasanii wa Nigeria.

Licha ya shambulizi hilo zito la maneno kutoka kwa Shatta Wale, Burna Boy alisema bado amejitolea kuijenga Afrika yenye nguvu zaidi, akisema “Hakuna mtu atakayeharibu umoja tunaojaribu kuujenga kwa Afrika yenye nguvu na bora zaidi.”

Kabla ya mahusiano yao kuvurugika, Burna Boy aliwahi kushirikishwa na Shatta Wale  kwenye wimbo ‘Hossana’ uliotoka mnamo mwaka 2017.

Umri wa mwisho wa mwanamke kuolewa...
Bunge la Afrika Kusini lateketea kwa moto