Mshambuliaji na nahodha wa Man Utd Wayne Rooney amesema ataendelea kubaki na klabu hiyo, licha ya kuhusishwa na taarifa za kuwa mbioni kutimkia nchini China.

Rooney ametoa kauli hiyo saa 24 baada ya vyombo vya habari kuripoti wakala wake Paul Stretford amesafiri kuelekea China kwa ajili ya kufanya mazungumzo na baadhi ya klabu ambazo zipo tayari kuiwania saini yake.

Klabu za Beijing Guoan na Jiangsu Suning ambazo zilitajwa kuwa katika harakati za kumsajili Rooney zimekanusha uvumi huo.

Kwa upande mwingine meneja wa klabu ya Tianjin Quanjian ambayo ilitajwa kwenye mlolongo huo Fabio Cannavaro alikua wa kwanza kukanusha taarifa za kumnyemelea Rooney.

Rooney amesema hana sababu ya kuondoka Man Utd katika kipindi hiki, kutokana na kutambua umuhimu wake ndani ya kikosi cha Mashetani wekundu, hivyo ataendelea kupambana ili afanikishe azma ya kurejeshwa katika kikosi cha kwanza.

Rooney anaeshikilia rekodi ya kuwa mfungaji bora wa muda wote wa Man Utd kwa kufunga mabao 250 katika michezo 546 aliyocheza, alisajiliwa klabuni hapo mwaka 2004 akitokea Everton kwa ada ya uhamisho ya Pauni milioni 27 akiwa na umri wa miaka 18.

Spurs Fungu La Kukosa, Yatolewa Europa League
Video: Mbowe na Wema waungana kortini, Chuo Kikuu chaipinga TCU