Waziri wa Madini nchini Dkt. Doto Biteko amesisitiza kuhusu utekelezaji wa Mkataba wa Makubaliano baina ya nchi ya Tanzania na Burundi katika kubadilishana ujuzi wa mnyororo mzima wa Sekta ya Madini nchini.

Dkt.Biteko ameyasema hayo Oktoba 28, 2022 mkoani Dodoma alipokutana na ujumbe maalum kutoka Jamhuri ya Burundi katika hafla ya kuuaga ujumbe huo baada ya kumaliza ziara ya siku sita nchini ya kujifunza kuhusu usimamizi na maendeleo ya Sekta ya Madini nchini.

Dkt.Biteko ameendelea kuushukuru ujumbe huo na kusema kuwa amefurahishwa na ugeni huo na anaamini kuwa yote yaliyokubaliana nayo yatafanyika kwa ushirikiano kwa lengo la kupanua mipaka ya ushirikiano Katika sekta ya Madini.

Kwa upande wake, kiongozi wa ujumbe huo ambaye pia ni mshauri wa Rais Katika masuala ya Madini nchini Burundi Alphonsia Kwizera , ameipongeza serikali ya Tanzania kuwa na sera nzuri za kuiendeleza Sekta ya Madini na usimamizi mzuri wa sekta ya madini kwa wachimbaji wadogo na wa kati.

Naye, Katibu Mkuu wizara ya Madini Adolf Ndunguru amepongeza ujumbe huo na kutumia siku zote sita walizotumia kujifunza masuala ya Sekta ya Madini nchini na kufafanua kuwa kujifunza hakuna mwisho hivyo Tanzania na Burundi zitaendelea kubadilishana uzoefu kwasababu maswala ya kupeana ujuzi ni makubaliano ya pande mbili.

Ziara hii ni matokeo baada ya Tanzania na Burundi kusaini makubaliano juu ya ushirikiano Katika usimamizi wa rasilimali madini.

Tishio la ugaidi: Polisi yaimarisha usalama
Korea kumuunga mkono Rais Samia ujenzi Chuo cha TEHAMA