Kiungo wa Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Young Africans Feisal Salum Abdallah (Fei toto) leo Alhamis (Desemba 29) ameichezea Klabu yake ya zamani JKU dhidi ya ya Mlandege, Uwanja wa Mao Zedong kisiwani Unguja ‘Zanzibar’.

Mchezo huo wa Kirafiki umeshuhudua JKU aliyoitumikia Fei Toto kwa mara ya kwanza baada ya kuacha gumzo kwa Mashabiki wa Soka nchini Tanzania, ikiibuka na ushindi Mabao 4-2.

Kiungo huyo alitumia dakika 45 za kipindi cha pili, ambapo aliikuta JKU ikiwa nyuma kwa Mabao 2-0, lakini uwepo wake ulisaidia kupatikana kwa ushindi huo mkubwa, huku akifunga bao moja.

Baada ya mchezo huo Mwandishi wa Habari Abubakar Kisandu alizungumza na ‘Fei Toto’, lakini alishindwa kupata ukweli wa kile alichokikusudia kutokana na muhusiska kuweka masharti ya kuulizwa swali lolote linalohusu sakata lake na Young Africans.

“Naomba nisiongee chochote, naomba sana, ikifika siku ya kuongea nitaongea “. Alisema Fei.

Si mara ya kwanza Fei kuonekana kucheza JKU kwani ndio Klabu iliyomkuza hadi alipohamia Tanzania Bara mwaka 2018, akitimkia Singida United na baadae kujiunga na Young Africans.

Jumamosi ya Disemba 24, 2022 kupitia mitandao yake ya Kijamii Fei aliwaaga Wanayanga huku timu yake hiyo siku hiyo hiyo ikitoa taarifa yakuwa bado Fei ana mkataba na Yanga mpaka Mei 30, 2024.

Hivi karibuni ziliibuka taarifa ya kuwa ‘Fei Toto’ huenda akajiunga na Azam FC kutokana na dau nono aliloahidiwa ambapo yeye binafsi aliwahi kusema hachezi mpira kufurahisha Watu bali anacheza Soka kwa kuangalia wapi kuna maslahi.

Roberto Oliveira ang'oka Vipres SC
PICHA: Young Africans waifuata Mtibwa Sugar Morogoro