Kamati ya Bunge ya Madini imewasilisha ombi la kutaka Bunge limuite Rais wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe kujibu tuhuma za upotevu wa mapato ya dola za Kimarekani bilioni 15 kwenye sekta ya madini.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Temba Mliswa ameibua suala la mapato hayo kwenye sekta ya madini ikiwa ni miezi michache tangu Mugabe aondoke madarakani.

Miaka miwili iliyopita, Mugabe akihutubia taifa kupitia televisheni ya taifa alisema kuwa nchi hiyo imeingiza kiasi cha dola za kimarekani bilioni 2 kwa mauzo ya almasi, lakini makadirio yanaonesha kuwa nchi hiyo ilipaswa kuingiza dola za kimarekani bilioni 15.

Mliswa alihoji kwanini Serikali ya Mugabe iliamua kuondoa makampuni kwenye migodi ya almasi na kuipa nafasi Serikali kufanya biashara ya madini ya almasi Februari 2016.

“Kama tutaweza kumuita rais wa zamani hapa, atatuambia kwanini Serikali iliamua kuchukua migodi ya almasi kutoka kwa wawekezaji wakati walikuwa bado wamewekeza fedha zao,” Mliswa anakaririwa na New Zimbabwe.

Mugabe alilazimika kujiuzulu nafasi yake ya Urais Novemba mwaka jana baada ya jeshi kuingilia kati mgogoro wa kisiasa ndani ya chama tawala cha ZANU-PF.

Ajali yaua watano na kujeruhi tisa
Museveni awatumbua Mkuu wa Polisi, Waziri wa Ulinzi kukomesha utekaji