Kocha mkuu wa mabingwa wa soka Tanzania bara Young Africans George Lwandamina wamewatahadharisha mashabiki wa klabu hiyo kwa kuwaambia wasitarajie matokeo ya mteremko katika mchezo wa kesho wa ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya Zanaco FC, kwa kigezo cha kuwa na mazoea na soka la Zambia.

Lwandamina amesema ni vigumu kutambua mbinu mpya za kikosi cha klabu hiyo ambacho kiliwasili jana alasiri kikitokea nchini kwao Zambia.

Amesema wakati mwingine mashabiki  wa soka wanaweza kumbebesha mzigo kocha mkuu kwa kuhisi mazingira anayotoka yanaweza kutambua mbinu za timu pinzani jambo ambalo sio la kweli.

“Nimeondoka Zambia kwa miezi kadhaa sasa, sijawahi kuiona Zanaco ikicheza kwa siku za karibuni, sijui mbinu zao mpya wala miakakati yao wanayoitumia kwa ajili ya kupata ushindi, lakini nimekiandaa kikosi changu kucheza kwa ushindani.”

“Young Africans imejiandaa kwa ajili ya kupambana jumamosi, hatuwezi kushinda kupitia vyombo vya habari, tutatumia juhudi zetu kuhakikisha tunapata matokeo mazuri.” Alisema Lwandamina

Kuhusu madai ya benchi la ufundi la Zanaco ya kusema wanamtambua vizuri Lwandamina pamoja na mbinu zake anazotumia uwanjani, kocha huyo kutoka Zambia amesema suala hilo hadhani kama lina ukweli, kwa sababu yeye ni kocha na ana uwezo mkubwa wa kubadilisha mbinu kila kukicha hususan anapokua na kikosi kipya.

Xabi Alonso Kustaafu Soka
Bulembo awaaga wajumbe wa Jumuiya ya Wazazi CCM