Watanzania wanaoishi nje ya nchi wametakiwa kuzingatia sheria za Taifa husika na kamwe wasijihusishe na biashara haramu ya dawa za kulevya.

“Vita ya dawa za kulevya ni kubwa, hata hivyo Serikali tunaendelea kupambana nayo. Nchi ilikuwa inapoteza vijana ambao walikuwa wamejiingiza katika biashara haramu ya dawa za kulevya. Nawaomba msithubutu kuingia huko mtafungwa,” amesema.

Hayo yamesemwa na Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa leo Machi 22, 2017 wakati akizungumza na Umoja wa Watanzania wanaoishi nchini Mauritius katika mkutano alioutisha kwenye hoteli ya Meridien mjini Port Louis.

Majaliwa amesema katika kudhibiti biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya Serikali iliamua kuunda Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) na inafanya kazi vizuri. “Na tutakamata kila mtu anayejihusisha na biashara hiyo bila kujali cheo, uwezo na mamlaka aliyonayo,”.

Aidha, Watanzania hao walioko nchini Mauritius wametakiwa kujenga mshikamano wa pamoja na wawe na uzalendo na nchi yao. Pia wawe mabalozi wazuri wa kutangaza vivutio vya Taifa.

Naye, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Khalid Salum Mohammed amewaomba Watanzania hao wazidishe mshikamano miongoni mwao kwa kuwa umoja wao ndiyo nguzo yao.

“Mko hapa kwa ajili ya kutafuta elimu na wengine mnafanya kazi, shughuli ambazo  zitawasaidia kuboresha maendeleo yenu na Taifa kwa ujumla, hivyo nawaomba mzingatie kilichowaleta,” amesema.

Pia, Mwenyekiti wa muda wa Umoja wa Watanzania waishio nchini Mauritius, Donald Kongwa ambaye ni Ofisa wa benki ya Standard Chaetered nchini Mauritius amemuhakikishia Waziri Mkuu kwamba kipato wanachokipata watakitumia kwa kuwekeza Tanzania kwa lengo la kukuza uchumi wa Taifa.

Aidha, amesema wanaunga mkono na kupongeza jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika  kujenga uchumi wa viwanda, mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, ujenzi wa miundombinu ya kisasa, ununuzi wa ndege pamoja na kuimarisha uwajibikaji na nidhamu kwa watumishi wa umma.

Magazeti ya Tanzania leo Machi 23, 2017
FC Barcelona Vs Real Madrid Ni Zaidi Ya Fainali Ya UEFA