Baada ya kutwaa ubingwa wa kombe la ligi (EFL Cup), meneja wa Man Utd Jose Mourinho ameanza mipango ya kuhakikisha mshambuliaji wake kutoka nchini Sweden Zlatan Ibrahimovic, anakubalia kusaini mkataba mpya.

Mourinho amesisitiza jambo hilo mbele ya waandishi wa habari baada ya mchezo wa fainali ya kombe la ligi kumalizika kwa kuifungwa Southampton mabao matatu kwa mawili.

Ibrahimovic, mwenye umri wa miaka 35, alijiunga na Man Utd wakati wa majira ya kiangazi baada ya kuwa huru, kufuatia kumaliza mkataba wake na mabingwa wa soka nchini Ufaransa Paris-St Germain.

Mshambuliaji huyo ambaye aliiwezesha Man utd kutwaa ubingwa wa kombe la ligi (EFL Cup) hapo jana kwa kufunga bao la ushindi, alisaini mkataba wa mwaka mmoja.

Mpaka sasa ameshafunga mabao 26 katika michezo 38 ya michuano yote aliyoitumikia Man Utd, hali ambayo inamuaminisha Mourinho huenda akapata makubwa zaidi ya hayo, endapo ataendelea kufanya nae kazi huko Old Trafford.

“Sisi sote tunataka abaki ili aendelee kuitumikia Man Utd kwa kipindi kingine, hakuna atakaependezwa na kuondoka kwake kama itatokea,”

“Kwa sasa nipo katika mazungumzo ya kina dhidi yake ili kuangalia uwezekano wa kumsainisha mkataba mpya, nina uhakika akiendelea kubaki hapa, Man utd itapata mafanikio makubwa zaidi, kutokana na umahiri wake wa kucheza soka la kufunga mabao” Alisema Mourinho.

“Sijawahi kumuomba mchezaji asaini mkataba mpya katika maisha yangu ya ukufunzi wa soka, lakini kwa Zlatan inanilazimu kufanya hivyo kutokana na umuhimu wake kikosini.” Aliongeza Mourinho.

Mpaka sasa Ibrahimovic ameshashinda mataji 32 tangu alipoanza kucheza soka la kulipwa mwaka 1999.

Ruvu Shooting Waapa Kuizika Yanga
Pepe Mel Afikiriwa Estadio Riazor