Aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu Bingwa Tanzania Bara Simba SC Ismail Aden Rage ameibuka na kuwatahadharisha Viongozi, Wanachama na Mashabiki wa klabu hiyo kuhusu Kocha Mpya Pablo Franco Martin.

Rage ambaye kwa sasa ni Mwanachama wa kawaida wa Simba SC amesema Kocha huyo kutoka nchini Hispania hapaswi kupimwa na mchezo wa watani wa jadi ambao unatarajiwa kupigwa Disemba 11.

Rage ambaye pia amewahi kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Soka nchini ‘FAT’ kwa sasa Shirikisho ‘TFF’ amesema anaamini kocha Pablo atafanya vizuri kama makocha waliomtangulia kwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

“Pablo ana wasifu mzuri na naamini viongozi wamepiga hatua na kutambua timu inahitaji kocha wa aina gani lakini wanatakiwa wasiingilie mipango yake, wamsikilize ili waone alichokuja nacho, naamini furaha itarejea lakini mashabiki na wanachama wanatakiwa kufahamu kuwa kazi ya kocha inapaswa kuheshimiwa na kupewa muda.” amesema Rage.

Pia Rage amesema japokuwa mchezo wa watani wa jadi kila mmoja anapenda kushinda kutokana na utani wao, lakini Kocha Pablo hapaswi kupimwa kwa mchezo huo kwani mafanikio hupimwa kwa mataji na siyo kufungwa.

Kocha Pablo mwenye umri wa miaka 41 aliwasili Jijini Dar es salaam Juzi Jumatano (Novemba 10) tayari kuanza majukumu yake wakati na mchezo wake wa kwanza wa Ligi Kuu ni dhidi ya Ruvu Shooting uliopangwa kupigwa Novemba 19.

Kocha Pablo ambaye amewahi kuwa Kocha msaidizi wa Real Madrid amesema amefurahi kujiunga na Simba SC kutokana na ukubwa wa klabu hiyo katika barani Afrika pamoja na kuwa na mashabiki wengi.

Kocha huyo jana Alhamis (Novemba 11) alikuwa jukwaani akiangalia viwango vya wachezaji wake walioanza kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichocheza dhidi ya DR Congo katika mpambano wa kuwania kufuzu fainali za Kombe la Dunia 2022.

Wachezaji wa Simba SC ambao walianza kwenye kikois cha Taifa Stars ni Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohamed Hussein, Denis Kibu, Kennedy Juma, huku John Bocco, Erasto Nyoni, Mzamiru Yassin walitumika kama wachezjai wa akiba.

Kabla ya kujiunga na Simba Kocha Pablo alikuwa anaifundisha Al Qadsia SC ya Kuwait kuanzia 2019 hadi 2021. Mwaka 2015 alikuwa kocha mkuu wa Getafe CF inayoshiriki Ligi Kuu Hispania pia alikuwa kocha msaidizi wa Real Madrid 2018 chini ya kocha Julen Lopetegui na baadaye Santiago Solari.

Tanzania Prisons yatangaza tahadhari Ligi Kuu
Jenerali ajiteua kuongoza Srikali ya Mpito Sudan