Uongozi wa Tottenham Hotspur umeongeza majina mawili zaidi kwenye orodha ya makocha wanaosakwa klabuni hapo, kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa Ligi Kuu ya England mwezi August, imeelezwa.

Spurs imekuwa haina Kocha mkuu tangu ilipomfuta kazi Antonio Conte, mwezi Machi mwaka huu.

Kiungo wa zamani wa timu hiyo, Ryan Mason ndiye anayesimamia timu hiyo kwa sasa baada ya awali kuachiwa aliyekuwa msaidizi wa Conte, Cristian Stellini, ambaye pia alifukuzwa baada ya mechi nne tu akiwa kocha wa muda.

Lakini, bosi wa Spurs, Daniel Levy anataka ampate Kocha mpya kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa 2023-24 na kinachoelezwa ni kwamba kwenye orodha amejumuishwa kocha wa Brentford, Thomas Frank juu ya mpango wa kupewa kibarua hicho.

Frank amekuwa akifanya vizuri Brentford tangu alipoteuliwa Oktoba 2018 Kufuatia kuondoka kwa Dean Smith.

Spurs pia imemwongeza kocha wa Inter Milan, Simone Inzaghi kwenye mchakato huo na imeelezwa kuwapo na mawasiliano baina ya pande hizo mbili.

Orodha ya awali ya makocha waliokuwa wakitajwa kwenye mchakato huo wa kupewa kibarua cha kuinoa Spurs ni pamoja na Xabi Alonso, Arne Slot, Brendan Rodgers na Graham Potter.

Kocha wa zamani wa Bayern Munich, Julian Nagelsmann amejiweka pembeni.

Zifahamu sababu za wenyeji wa Songea kuitwa Wangoni
Mtibwa Sugar: Tutang'ang'ana hadi mwisho