Kamishna wa Uhamiaji, Uraia na Pasipoti, Gerald Kihinga amesema kuwa mtu atakayepoteza hati ya kusafiria inayopatikana kwa sh. 150,000 atalazimika kuipata kwa sh. 500,000 kupata nyingine.

Hayo yamesemwa na kamishna wa Uhamiaji katika uzinduzi wa utoaji wa hati hizo Jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa gharama hiyo itasaidia watu kutunza hati zao.

Amesema kuwa zipo kesi nyingi za watu kupoteza hati zao za kusafiria na baadhi yake ni zile zinazotokea katika matukio yasiyohitaji uwepo wake.

“Utakuta mtu anakuja kuomba hati mpya, ukimuuliza mazingira ilivyopotea anasema alikuwa akielekea Kariakoo kutoka Buguruni, sasa huko Kariakoo hati hiyo unaenda nayo ya nini? Tuzitunze hati hizi kwa sababu ni nyaraka muhimu kwa nchi yetu,” amesema Kihinga.

Aidha, amefafanua kuwa hakuna haja ya kuzunguka na hati hiyo kila mahali isipokuwa yale maeneo muhimu yanayohitaji ili kuepuka gharama kubwa inapopotea.

Hata hivyo, Kamanda wa Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam, Chrispin Ngonyani amesema kuwa upo udhibiti wa kutosha kuhakikisha kila anayeomba hati hiyo anapewa kwa wakati bila bugudha wala usumbufu wowote.

Makala: Wimbo wa Mpoto ulihitaji kiki ya uongo ya MC Pilipili na ..?
JPM atoa shavu jingine Bima (TIRA)