Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) limeeleza kuwa wimbo wa Nay wa Mitego uliosambaa kwenye mitandao hivi karibuni ukiwa na jina la ‘Wapo’ una matusi na haufai.

Katibu Mkuu wa Basata, Godfrey Mngereza ameeleza kuwa Baraza liliusikiliza wimbo huo na kubaini kuwa ni wimbo usiofaa kwa jamii na zaidi unachochea vurugu.

“Ule wimbo tumeusikiliza, kama Baraza tunasema ule wimbo hauna maadili, ni wimbo ambao una matusi, ni wimbo ambao unachochea vurugu, ni wimbo ambao haufai kwa jamii,” alisema.

Aliongeza kuwa vyombo vyote vya habari ambavyo vitaucheza wimbo huo vitakumbwa na mkono wa sheria kutoka kwa vyombo husika.

Nay wa Mitego alikamatwa na Jeshi la Polisi Mkoani Morogoro majira ya saa nane usiku, na lifikishwa Dar es Salaam anakoshikiliwa kwa mahojiano na Jeshi la Polisi.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi Mkoani Morogoro, Kamanda Ulrich Matei alithibitisha kukamatwa kwa msanii huyo usiku wa kuamkia jana.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, wakili Peter Kibatala amesema kuwa atasimamia kesi dhidi ya msanii huyo na kwamba tayari ameshamjulia hali katika kituo cha kati jijini Dar es Salaam.

Maafisa Habari watakiwa kutoa haraka habari za Serikali kwa Umma
Mayanga: Erasto Nyoni Ni Bora Zaidi Ya Kelvin Yondani