Kiungo Mshambuliaji kutoka nchini Ghana Bernard Morrison ameonesha bado ana mapenzi na Klabu ya Simba SC, licha ya kuhusishwa na mpango wa kusajiliwa na Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Young Africans.

Morrison anatajwa kukamilisha dili la kurejea Young Africans, kufuatia mkataba wake na Simba SC kutarajia kufikia kikomo Agosti 30, huku Uongozi wa Msimbazi ukimpa mapumziko hadi mwishoni mwa msimu huu 2021/22.

Kiungo huyo ambaye amekua kivutio cha wadau wengi wa soka Tanzania kutokana na vibweka vyake, amedhihirisha bado anaipenda Simba SC, kufuatia ujumbe aliouandika kwenye ukurasa wake wa Instagram, akiomba mchango wa manunuzi ya jezi za klabu hiyo.

Morrison anaomba msaada huo kwa ajili ya kuzigawa kwa Mashabiki na Familia nchini kwao Ghana.

Morrison ameandika: Mara nyingi tunakatishwa tamaa na wale tunaowapenda na kuwaamini. Lakini wacha nifanye hadithi yangu kuwa fupi na rahisi, nahitaji jezi 100 za Simba SC kutoka kwa mashabiki waaminifu kwa ajili ya marafiki na familia nchini Ghana. 

Hii ni kutokana na nyinyi mashabiki kuniaga kwa sababu nitakatishwa tamaa ikiwa nitaendelea kusubiri kupata moja kutoka kwa klabu yangu.  tafadhali andika jina lako nyuma na namba 3.

Okrah aomba radhi Ghana, ajutia kadi nyekundu
Mbunge wa zamani Ole Telele kuhamia Msomera