Rais wa mabingwa wa soka nchini Hispania na barani Ulaya (Real Madrid) Florentino Perez, ameshindwa kujizuia na kutangaza hadharani namna anavyomuhusudu kiungo mshambuliaji wa Chelsea Eden Hazard.

Perez amesema anampenda sana kiungo huyo kutokana na umahiri wake anapokuwa uwanjani na angependa siku moja kumuona akiwa miongoni mwa wachezaji wataokisaidia kikosi chake, kufikia malengo ya kuendelea kutwaa ubingwa wa Hispania, Ulaya na ikiwezekana duniani.

Rais huyo amefunguka kuhusu Hazard alipohojiwa na kituo kimoja cha redio cha mjini Madrid, baada ya kuulizwa mipango ya usajili aliyonayo kwa sasa.

Perez amesema kama atapewa hitaji na kocha wake Zinedine Zidane la kumsajili Hazard, hatosita kufanya hivyo kwa sababu hata yeye anatamani kumuona akitua Santiago Bernabeu.

Kuhusu mshambuliaji wa mabingwa wa soka nchini Ufaransa AS Monaco Kylian Mbappe, kiongozi huyo amedai kuwa anaweza kufanikisha usajili wa mchezaji huyo wakati wowote endapo atahitaji kufanya hivyo, lakini akasisitiza kwanza anataka kumuona Hazard akivaa uzi wa Real Madrid kwanza.

Hazard alikua anahusishwa na mpango wa kusajiliwa na Real Madrid tangu msimu uliopita, lakini kipindi hiki cha usajili wa majira ya kiangazi tangu kilipoanza taarifa hizo zimefifia na bado haijafahamika kwa nini imekua hiyo.

Dkt. Mpango awatuliza wamachinga, awaahidi makubwa
Aubameyang aweka wazi hisia zake kwa klabu ya Chelsea