Serikali imsema itapitia upya sababu za kuanzishwa kwa Mamlaka ya Bonde la Mto Rufiji (RUBADA) kufuatia mamlaka hiyo kuendeshwa kwa ubabaishaji, kushindwa kusimamia uendelezaji wa bonde hilo na kusababisha malalamiko kutoka kwa wananchi.
Uamuzi huo wa Serikali umetolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Ikwiriri mkoani Pwani.
Majaliwa amesema baada ya mapitio hayo shughuli za mamlaka hiyo zitahamishiwa kwenye mamlaka nyingine za serikali kwani RUBADA imeshindwa kufanya kazi hiyo kwa muda mrefu.
“RUBADA wamepewa ardhi lakini wameshindwa kuiendeleza, tutafanya upya mapitio ya kuanzishwa kwake,” – Majaliwa
Waziri Mkuu pia ameitaka Kampuni ya Agro Forestry Plantation inayotaka kujenga kiwanda cha sukari wiyani Rufiji kuhakikisha asilimia 60 ya watumishi watakaowaajiri wawe ni vijana wa wilaya hiyo.
Aidha, Waziri Mkuu amepokea malalamiko kutoka kwa wananchi wa Ikwiriri kuhusu kutotatuliwa kwa mgogoro wa mpaka kati ya Wilaya ya Mkuranga na Ikwiriri.
Kufuatia taarifa hizo za mgogoro Waziri Mkuu amemuagiza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Willium Lukuvi, kwenda wilayani Rufiji kutatua mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu ambapo Mkurugenzi wa halshauri ya wilaya hiyo, Rashidi Salum alimweleza Waziri Mkuu kuwa, mgogoro huo umeshatatuliwa kwa ngazi ya wilaya hivyo hatua iliyosalia ni kwa Waziri wa Ardhi kufika na ramani ili kutoa uamuzi.