Michezo ya mkondo wa pili wa 16 bora ya ligi ya mabingwa barani Ulaya inaanza kurindima hii leo katika viwanja viwili tofauti.

Huko Emirates Stadium kaskazini mwa Jijini London, Wenyeji Arsenal wanapaswa kupindua kipigo cha mabao matano kwa moja walichoshushiwa na FC Bayern Munich katika Mchezo wa mkondo wa kwanza uliochezwa majuma mawili yaliyopita huko Ujerumani.

Ili kufanikisha azma ya kufuzu hatua ya robo fainali, Arsenal watalazimika kusaka ushindi wa mabao manne kwa sifuri ama zaidi.

Mchezo mwingine wa 16 bora wa ligi ya mabingwa barani Ulaya utachezwa huko mjini Naples nchini Italia, ambapo SSC Napoli watapambana na mabingwa watetezi Real Madrid.

Napoli watahitaji kusaka ushindi wa mabao mawili kwa sifuri ili kufanikisha safari yao ya kusonga mbele, baada ya kufungwa mabao mawili kwa moja katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliochezwa mjini Madrid majuma mawili yaliyopita.

Kesho, Jumatano michezo mingine miwili ya 16 bora ya michuano hiyo itachezwa, ambapo mabingwa wa soka nchini Hispania FC Barcelona watatunishiana msuli na mabingwa wenzao kutoka Ufaransa Paris Saint Germain.

Katika mchezo wa mkondo wa kwanza FC Barcelona walikubali kubanjuliwa mabao manne kwa sifuri.

Mchezo mwingine wa kesho utakua kati ya Borussia Dortmund dhidi ya Benfica ambao wapo mbele kwa bao moja walilolipata wakati wa mchezo wa mkondo wa kwanza.

Tanesco kuweka hadharani deni la Zanzibar
Tundu Lissu aachiwa kwa dhamana