Beki wa Kati wa Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Young Africans Ibrahim Abdullah ‘Bacca’ amesema ubora wa safu ya ulinzi wa kikosi chao ndio siri ya mafanikio huku akimtaja Yanick Bangala kuwa kiongozi, lakini akicheza namba sita.

Young Africans inayoundwa na ukuta wa Joyce Lomalisa, Dickson Job, Bakari Mwamnyeto, Bacca, Djuma Shaban, Kibwana Shomari na Yanick Bangala imeruhusu mabao 13 msimu huu 2022/23.

Bacca amesema anafurahi kucheza na mabeki wote waliopo Young Africans kutokana na kila mmoja kuwa na aina yake ya uchezaji huku akisisitiza kuwa anafurahi zaidi akicheza na Bangala kama namba sita.

“Mabeki wote nimepata nafasi ya kucheza nao wana uwezo na ni viongozi wazuri kiwanjani lakini nafurahi zaidi nikicheza na beki mwingine kati na Bangala akawa juu kama namba sita ni mtu makini sana na anapenda kuzungumza mimi namuita beki kiongozi,”

“Mkicheza uwanjani kwa kukumbushana majukumu mchezo wa mpira ni mwepesi na makosa mengi yanapungua tuna nahodha Mwamnyeto anazungumza ana kila sifa ya kuwa kiongozi lakini kuna Bangala hapendi timu ifungwe kizembe.” Amesema Bacca

Bacca amesema uimara wa safu yao ya ulinzi unajengwa na kuelewana vizuri na kukumbushana majukumu wawapo uwanjani huku akisisitiza kuwa kila mchezaji aliyepo kwenye safu hiyo ana ubora wake.

“Siwezi kutaja sifa za kila mchezaji ila kile kinachoonekana uwanjani kinatokana na kuaminiana na kupeana maelekezo ili kila mmoja aweze kufanya kwa ubora na timu ipate matokeo mazuri.” Amesema

Bacca alisajiliwa Young Africans wakati wa Dirisha Dogo msimu wa 2021/22 akitokea KMKM ya Zanzibar, baada ya kuonesha kiwango safi kwenye Michuano ya Kombe la Mapinduzi mwaka 2022.

Ujazo wa Maji Bwawa la JNHPP wafikia lita Bilioni sita
Makala: Usiyoyajua kuhusu Muungano wa Tanganyika, Zanzibar