Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetangaza mkakati utakaoiwezesha Timu ya Taifa ya Soka ‘Taifa Stars’ kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika ‘AFCON 2027’ na Fainali za Kombe la Dunia 2030.

Serikali imetangaza mkakati huo kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, ambapo imepanga kuunda Bodi ya ushauri ambayo itakua na jukumu la kuhakikisha kila hatua inafanyiwa kazi kiufundi na kiutekelezaji.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengelwa amesema tayari wameshaanza kuweka mikakati mbalimbali itakayosaidia kuiwezesha Tanzania kushiriki michuano hiyo mikubwa kwa kipindi cha miaka minane ijayo.

Amesema wataunda Bodi huru ya ushauri, ambayo itakuwa na Kocha atakayelipwa na Serikali na hatatakiwa kuingiliwa na mtu yeyote wala shirikisho la Soka ‘TFF’.

“Serikali itaunda bodi ya ushauri kwa ajili ya kushiriki Fainali za Kombe la Dunia 2030 na Fainali za Mataifa ya Afrika ‘AFCON 2207’, tutakuwa na kocha ambaye analipwa na Serikali na huyo Kocha asiingiliwe na mtu yeyote wala Shirikisho ” alisema waziri Mchengelwa

Tanzania haijawahi kushiriki Fainali za Kombe la Dunia tangu ilipojiunga na Shirikisho la soka la Kimataifa ‘FIFA’ mwaka 1964, lakini imewahi kushiriki Fainali za Mataifa ya Afrika ‘AFCON’ mwaka 1980 zilizofanyika nchini Nigeria na 2019 zilizofanyika nchini Misri.

AU yapendekeza msaada wa kifedha kwa Ukraine
Simba SC yakazia salamu za Mo Dewji