Hatimaye mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mwaka huu ametangazwa muda mfupi uliopita. Shirika la Kimataifa la Kampeni ya Kukomesha Matumizi ya Silaha za Nyuklia (ICAN) limetangazwa kushinda tuzo hiyo.

Akiitangaza ICAN kushinda tuzo hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Nobel, Berit Reiss-Andersen amesema kuwa shirika hilo limefanya kazi kubwa kusaidia kukomesha matumizi ya silaha hizo.

“Tunaishi katika dunia ambayo hatari ya matumizi ya silaha za nyuklia ni kubwa zaidi ya ilivyokuwa miaka mingi iliyopita,” amesema Mwenyekiti huyo.

Aliutaja mpango wa Korea Kaskazini kama tishio kubwa zaidi katika kipindi cha hivi karibuni na kuzitaka nchi zinazohusika kuanza mazungumzo ya kuondoa matumizi ya silaha hizo.

ICAN ni muungano wa taasisi zisizo za kiserikali kutoka nchi zaidi ya 100 duniani kote  zinazofanya kazi pamoja kujaribu kukomesha matumizi ya silaha za nyuklia. Makao makuu ya Shirika hilo yako Geneva Uswisi.

Tuzo hizo za kimataifa zilianzishwa mwaka 1895 na raia wa Sweden, Alfred Nobel. Mwaka 1901 tuzo hiyo ilitolewa kwa vipengele vya Kemia, Amani, Fizikia, Uandishi, Saikolojia na Madawa.

Bulaya: Ninafuatiliwa na watu waliovaa mavazi ya kininja
Video: Ujerumani yafuzu kombe la dunia 2018