Goli kipa aliyewahi kutajwa kama mlinda mlango bora zaidi nchini kwa kipindi kirefu, Juma Kaseja ambaye sasa ni mlinda  ‘lango’ la Kagera Sugar, amevunja ukimya kuhusu tetesi za kunyemelewa na mwajiri wake wa zamani, Simba SC.

Kaseja ambaye jana aliiwezesha Kagera Sugar kuisambaratisha Simba kwa kichapo cha 2-1, hali iliyopelekea wekundu hao wa Msimbazi kuwapisha kileleni watani wao wa jadi Yanga SC, amesema kuwa yeye kazi popote.

“Mimi nimeshasema ninacheza sehemu yoyote na nitaishi sehemu yoyote ile ili mradi tumeelewana,” Kaseja aliiambia E-FM huku akisisitiza kuwa kwa sasa anajikita katika kuhakikisha timu yake inasonga katika nafasi za juu zaidi katika Ligi Kuu Tanzania Bara inayodhaminiwa na  Vodacom (VPL).

“Unajua hata nilipokuwa nakuja Kagera Sugar, watu walianza kusema mara ‘ooh kweli utaweza… mara utaweza kweli kuishi Kagera, lakini sasa ndipo nilipo nafanya kazi yangu,” aliongeza.

Jana, Kaseja alionekana kuwa na kiwango kizuri cha kulinda goli na kuwafunga midomo kwa muda wale waliokuwa wanamkosoa kwa kudai kuwa ameshuka kiwango na kwamba umri wake unapishana na kasi ya soka nchini.

Matokeo hayo yanaiweka Kagera Sugar katika nafasi ya tatu ya Msimamo wa Ligi ikiwa na pointi 45, ikiwa nyuma ya Simba yenye pointi 55, huku kilele cha Ligi hiyo kikikaliwa na Wana wa Jangwani, Yanga SC kwa pointi 56 baada ya kuivunja ngome ya Azam FC 1-0, Jumamosi iliyopita..

Simba SC kwa upande wake, imepania kurejea katika kilele cha Ligi hiyo lakini ili kuifanikisha ndoto yake inapaswa kupambana kushinda katika mechi yake ya Jumatatu ijayo dhidi ya Mbao FC ya jijini Mwanza.

Wakati Simba wakihaha kurudi Kileleni, Yanga wao watakuwa na jukumu la kucheza mchezo wa kimataifa na MC Alger ya Algeria katika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika.

Video: CCM kuanza mikakati ya ushindi 2020
Trump Aahidi Kuikalia Kooni Korea Kaskazini Peke Yake