Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Daniel Sillo ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa matumizi mazuri ya fedha za umma katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa lango la kuingilia wageni, barabara ya kilomita 47.2 na ujenzi wa Picnic Site kwenye Pori la Akiba Mkungunero.

Ameyasema hayo, wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali kwenye Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma.

“Tuipongeze Wizara ya Maliasili na Utalii kwa usimamizi mzuri wa fedha hizi za umma ambazo zinaleta tija katika suala zima la maliasili na utalii hapa nchini,” Sillo amesisitiza.

Amesema Wizara ya Maliasili na Utalii ilipata kiasi cha shilingi bilioni 90.2 ambapo bilioni 12.9 ilikabidhiwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na kisha kiasi cha shilingi milioni 672 kupelekwa Pori la Akiba la Mkungunero kwa ajili ya kuboresha eneo hilo ili kuvutia wawekezaji na watalii.

Amefafanua kuwa, uboreshaji wa miundombinu ya Pori ya Akiba la Mkungunero utafungua fursa za utalii nchini Tanzania na pia itaongeza uchangiaji wa Sekta ya Maliasili na Utalii kwenye pato la Taifa ambapo kwa sasa sekta hiyo inachangia takribani asilimia 17 ya pato la Taifa na asilimia 25 ya fedha za kigeni.

Naye, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja (Mb) Wizara ya Maliasili na Utalii ilifaidika na mgao wa fedha za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 ambapo ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 88.57 sawa na asilimia 98 ya mpango huo.

Amefafanua kuwa, Pori la Akiba Mkungunero ilitengewa kiasi cha shilingi milioni 672 na mpaka sasa fedha hizo zimepokelewa zote na zimepangwa kutekeleza miradi mitatu ambayo ni ujenzi wa lango la kuingilia wageni, barabara ya kilomita 47.2 na ujenzi wa Picnic Site.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, iko Wilayani Babati na inaendelea na ziara ya kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Ligi ya Mabingwa Afrika Mashariki kuunguruma Arusha
Kamati yakagua miradi pori la Mkungunero