Kiungo kutoka nchini Ufaransa Paul Pogba huenda akaukosa mchezo wa ligi kuu ya soka nchini England utakaochezwa saa kadhaa zijazo, ambapo kikosi chake kitapapatuana na majogoo wa jiji Liverpool.

Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 24 ameingia katika mashaka ya kuukosa mchezo huo unasubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka duniani kote, baada ya kuumia mazoezini jana.

Imefahamika Pogba ameumia mguu jana katika mazoezi ya mwisho viwanja vya Carrington na hakumaliza, ingawa bado hajaondolewa rasmi kwenye mchezo wa leo.

Pogba ambaye ni mchezaji ghali aliyesajiliwa Man Utd kwa dau la rekodi, Pauni Milioni 89 anapambana na hali yake ili awe fiti kuteremka Uwanja wa Old Trafford leo kucheza.

Man United itapoteza nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya England iwapo itafungwa na Liverpool ya kocha Mjerumani, Jurgen Klopp.

Pamoja na hayo, Pogba hakuonekana wakati kikosi cha Man United kinaingia kambini jana kwenye hoteli ya Lowry kuelekea mchezo wa leo.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24 amekuwa mchezaji muhimu kwenye kikosi cha Man United tangu awasili Old Trafford.

Lakini alitemwa kwenye kikosi kilichomenyana na Huddersfield na Sevilla, na akatolewa katika mchezo dhidi ya Tottenham na Newcastle. Pogba pia alikosekana kwenye mechi ya Kombe la FA Man United wakishinda dhidi ya Huddersfield mwezi uliopita kwa madai alikuwa mgonjwa.

Baada ya hapo akaanza mechi zote dhidi ya Chelsea na Crystal Palace na kuzima tetesi kwamba ametofautiana na kocha Mreno, Jose Mourinho.

Eric Bailly pia yuko shakani kuanza leo kwa mara ya kwanza tangu aumie Novemba na kufanyiwa upasuaji wa kifundo cha mguu, baada ya kutokea benchi mara mbili, lakini Anthony Martial atakuwa nje kwa maumivu ya pua.

Anaingia kwenye orodha ya majeruhi wengine akina Ander Herrera, Zlatan Ibrahimovic, Marcos Rojo na Daley Blind ambao wote wanakosekana kwa sasa.

Fahamu tafsiri sahihi ya kosa la uhaini na adhabu yake
Mexime: Wachezaji wanafanya makosa mengi