Rais wa Shirikisho la Soka nchini Ufaransa ‘FFF’ Noel le Graet ameomba radhi hadharani, kufuatia kauli isiyofaa aliyoitoa dhidi ya Gwiji wa soka nchini humo Zinedine Yazid Zidane.

Kiongozi huyo wa juu wa ‘FFF’ alitoa kauli hiyo alipohojiwa na Kituo cha Radio cha Ufaransa, akisema hata kama Zidane angempigia Simu kuhusu suala la kuomba kazi ya kukinoa kikosi cha nchi hiyo asingepokea.

Le Graet mwenye umri wa miaka 81 amesema hana budi kumtaka radhi Zidane kwa kauli hiyo, ambayo imepokelewa vibaya miongoni mwa wadau wa soka nchini Ufaransa.

“Ninapenda kuomba radhi kwa kauli yangu dhidi ya Zidane, ninaamini imeleta mtazamo tofauti miongoni mwa wadau wa soka wa nchi hii na Duniani kwa ujumla, kauli ile haikuwa ya Shirikisho, ilikua yangu binafsi na ndio maana ninaomba radhi mimi kama mimi,” amesema Le Graet.

“Nilifanya mahojiano na [redio ya Ufaransa] RMC ambayo sikupaswa kutoa kauli hiyo, lakini ilitokana na ubishani uliokuwa umechukua nafasi miongoni mwa Mashabiki wa Soka kuhusu Didier Deschamps na Zinedine Zidane, ambao wote kwa pamoja wamecheza soka na kufundisha kwa mafanikio makubwa.”

“Ninakubali kwamba nilitoa matamshi ya kutatanisha ambayo yalizua kutokuelewana kati yangu na baadhi ya wadau wa Soka hapa Ufaransa na Duniani kote.”

Mfungaji Bora katika Fainali za Kombe la Dunia 2022 na Mshambulizi wa Kikosi cha Ufaransa Kylian Mbappe, alikuwa wa kwanza kuonyesha kuchukizwa na kauli ya Kiongozi huyo na kuandika katika Ukurasa wake wa Mtandao wa Twitter kwa kuonyesha Le Graet alimkosea heshima Zidane: “Amekosewa heshima”.

Hata hivyo Waziri wa Michezo wa Ufaransa Amelie Oudea-Castera alitangulia kuomba radhi kwa Zidane, kufuatia kauli ya Le Graet kwa kuandika Mitandaoni “Inatia aibu kwa kushindwa kuonyesha heshima”.

Jumamosi (Januari 07) Shirikisho la Soka nchini Ufransa ‘FFF’ lilimsainisha mkataba mpya Kocha Didier Deschamps, ambao utaendelea kumuweka madarakani hadi mwaka 2026, kufuatia mafanikio aliyoyapata ya kutwaa ubingwa wa Dunia mwaka 2018 na kutinga Fainali mwaka 2022.

Zidane alikuwa miongoni mwa wachezaji walioipa ubingwa wa Dunia Ufaransa mwaka 1998 sambamba na Deschamps, na tayari Gwiji huyo ameshatwaa Ubingwa wa Ligi ya Hispania mara mbili pamoja na Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya Mara tatu mfululizo kabla ya kuondoka klabuni hapo mwaka 2022.

Kocha Simba SC amkataa John Bocco
Watanzania watakiwa kuadhimisha miaka 59 Mapinduzi Zanzibara kwa kupanda miti