Mfaransa Sebastien Migne ametangazwa kuwa kocha mkuu wa kikosi cha timu ya taifa ya Congo Brazzaville akichukua nafasi ya Pierre Lechantre.

Migne mwenye umri wa miaka 44, aliwahi kufanya kazi na kocha mkongwe barani Afrika Claude LeRoy alipokua akivinoa vikosi vya DR Congo na Togo.

Congo Brazzaville walikua hawajafanya maamuzi ya kumtangaza kocha mkuu wa kikosi cha timu yao ya taifa, tangu walipoachana na Lechantre mwezi Novemba mwaka 2016.

Migne, ambaye alifanya kazi kama kocha msaidizi wa timu ya taifa ya Togo wakati wa fainali za kombe la Afrika zilizochezwa mapema mwaka huu nchini Gabon, alikua miongoni mwa makocha wanne waliokua wanawania ya ajira huko Congo Brazzaville.

Wengine waliokua wanawania nafasi hiyo ni Patrice Neveu, John Toshack na Paul Put.

Migne, amesaini mkataba wa miaka miwili na atakua akilipwa mshahara na serikali ya Congo Brazzaville kupitia wizara ya michezo inayoongozwa na Léon-Alfred Opimbat.

Migne akiwa kama kocha msaidizi wa LeRoy alisaidia mafanikio ya kuifikisha DR Congo katika hatua ya robo fainali ya michuano ya Afrika ya mwaka 2015.

Jose Mourinho Aichimba Mkwara Real Madrid
TLS wamjibu Dkt. Mwakyembe kuhusu uchaguzi