Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema kuwa Tanzania ipo salama na imara na kwamba mtu yeyote atakayejaribu kutaka kuvuruga amani atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Majaliwa ameyasema hayo leo jijini Dar es salaam mara baada ya kukutana na kufanya mazungumzo kuhusu mambo mbalimbali yahusuyo mahusiano na Balozi wa Iran nchini Tanzania, Mousa Farhang.

“Hatua kali zitachukuliwa kwa yeyote kutoka popote atakayejaribu kuvuruga amani yetu, nawaomba wananchi muwe makini na muendelee kuidumisha amani yetu, fanyeni shughli zenu kwa amani bila vitisho vyovyote,”amesema Majaliwa

Amesema kuwa kwa sasa Serikali ipo katika mapambano dhidi ya vitendo vya ufisadi, rushwa, biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na wahujumu uchumi ambao wamekuwa wakuhujumu mali za umma.

Aidha, ameongeza kuwa mbali ya kuimarisha amani nchini, pia Serikali imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji jambo ambalo litawawezesha watakaokuja kuwekeza nchini kupata tija.

Hata hivyo, ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kutoka nchini Iran ili waje kuwekeza kwenye viwanda mbalimbali vikiwemo vya kuchakata mazao ya  kilimo.

 

Magazeti ya Tanzania leo Septemba 14, 2017
Video: Mlinzi wa Meja Jenerali Mstaafu Vicent ashikiliwa na Polisi