Jeshi la Polisi Kanda Maalum  ya Dar es salaam limewaonya wananchi ambao wanaojiandaa na maandamano yanayoratibiwa kupitia mitandao ya kijamii na kusema kwamba wasijaribu kufanya hivyo kwani wataingia kwenye matatizo makubwa.

Hayo yamesemwa na Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es salaam, Kamanda Lazaro Mambosasa wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo amewataka Watanzania wajiepushe na uchochezi huo wa watu wachache wa kutaka kuiingiza nchi kwenye vurugu.

Amesema kuwa kwa yeyote ambaye hatasikia onyo hilo kwa mkoa wa Dar es salaam asije kujutia kwa yatakayomtokea kwani jeshi limejipanga vilivyo na kwamba kwa sasa lipo kwa ajiili ya kutengeneza mazingira rafiki kwa wawekezaji.

“Kuna watu ambao wanaendelea kuhamasisha wananchi kuvunja sheria. Wanataka wajiandae kwa maandamano, tarehe wanazoendelea kutaja.  lakini wanafanya hivyo wao wakiwa wamekaa sehemu salama. Wanataka kuwaingiza watanzania wengine kwenye shida, sasa nawasihi wasiandamane, maana kitakachowatokea tusilaumiane,”amesema Kamanda Mambosasa

Hata hivyo, kumekuwa na vuguvugu la kufanyika kwa maandamano Aprili 26 huku mwanaharakati wa mitandaoni Mange Kimambi akionekana kuwa mstari wa mbele katika uhamasishaji.

 

Botswana yamlaumu Kabila kwa ghasia zinazoendelea DRC
Mch. Mwingira aibuka kidedea dhidi ya Mmarekani Mahakamani