Waziri wa Nchi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Selemani Jaffo ametangaza tarehe rasmi ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2019.

Ametangaza tarehe ya kufanyika uchaguzi huo Agosti 23 Jijini Dodoma wakati akitoa maagizo kwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa na Viongozi mbalimbali kuelekea uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika mwaka huu.

Ikiwa ni miezi minne imebakia kabla ya kumalizika kwa mwaka 2019, Waziri Jaffo amesema kuwa uchaguzi huo utafanyika, Novemba 24, ambapo zoezi la kupiga kura litaanza saa 2:00 Asubuhi hadi saa 10:00 Jioni.

Aidha, amesema kuwa Kampeni za uchaguzi zitafanyika siku saba kabla ya siku ya Uchaguzi, na kila chama kitakachoshiriki uchaguzi kitawasilisha ratiba yake ya Kampeni, si chini ya siku 7 kabla ya kuanza Kampeni.

“Ofisi ya Mkoa ndiyo itakuwa Mratibu Mkuu wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika Mkoa husika, ambapo Halmashauri za wilaya zitawajibika kuratibu Uchaguzi kwa mujibu wa maelekezo yaliyoonyeshwa katika Mwongozo, Kwa mujibu wa Kanuni hizi, viongozi waliochaguliwa katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliopita, ukomo wa Uongozi wao utakuwa ni siku 7 kabla ya siku ya kuchukua fomu kuanza kampeni,”amesema Jafo

Nchi tajiri duniani G7 zakutana, janga la moto msitu wa Amazon lahusishwa
Waziri Mwakyembe awatahadharisha TFF, 'Kuweni makini'