Mke wa aliyekuwa mgombea urais kupitia Chadema, Edward Lowassa, Mama Regina Lowassa ambaye alishiriki kwa kiasi kikubwa katika kukiongezea kura chama hicho na kuwapatia wabunge wengi kwa kuwashawishi wanawake hivi karibuni alitangaza kuikataa zawadi ya Ubunge wa viti maalum aliyepewa kwa heshima na chama chake hicho.

Ingawa Regina alikuwa mwanaharakati mkubwa wa kisiasa, alikataa kuingia katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sehemu ambayo wanasiasa wengi hutumia nguvu kubwa kuingia.

Kwa mujibu wa msemaji wa Lowassa, Abubakari Liongo, Regina Lowassa alichagua kuendelea kuwatumikia akina mama nje ya Bunge kwa kuwa anaamini atafanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi akiwa nje ya Bunge ambalo lingemuongezea majukumu mengi.

“Ninawashukuru Kamati Kuu ya chama changu kwa heshima hii kubwa waliyonipa na poia naithamini sana, lakini naamini nitaendeleza mapambano ya kuwaletea mabadiliko akina mama kwa ufanisi zaidi nikiwa nje ya Bunge,” Liongo alimnukuu mama Regina Lowassa.

Kutokana na kazi kubwa aliyoifanya Mama Regina Lowassa wakati wa Kampeni, imedhihirisha wazi kuwa alikuwa na sifa za kuwa mbunge.

Chadema wamejipatia viti maalum 36 katika Bunge la 11 linalotarajia kuanza rasmi Novemba 17 mwaka huu. Vyama vya Upinzani kwa ujumla vimepata nafasi ya kuwa na wabunge 116 katika Bunge la 11, idadi ambayo ni kubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa vyama vya vingi nchini.

 

Kung’arisha Mchele wa Mbeya Kwahatarisha Soko
Ukawa, Polisi Watofautiana Tena