Baraza la Sanaa, Sensa, Filamu na Utamaduni la Zanzibar, limemfungia msaanii wa kizazi kipya Zuhura Othman Masoud maarufu Zuchu kuendesha shughuli zote za sanaa visiwani Zanzibar sambamba na kupiga marufuku redio na televisheni za visiwani humo kupiga nyimbo zake kwa kipindi cha miezi sita.
Hatua hiyo imekuja baada ya tukio la Februari 24 mwaka huu Zuchu wakati akitumbuiza katika usiku wa Fullmoon Kendwa Mkoa wa Kaskazini Unguja kudaiwa kuimba nyimbo, kutoa matamshi na kuonyesha ishara mbaya ambazo ni kinyume na maadili ya kizanzibari.
Akizungumza leo Machi 5, 2024 ofisini kwake na waandishi wa habari, katibu mtendaji wa baraza hilo, Omar Abdalla Adam amesema baraza limemfungia kwa kipindi cha miezi sita kuanzia sasa.
“Baraza lina wajibu wa kusimamia mila, silka desturi na utamaduni wa Mzanzibari, kwa hiyo linatamka rasmi kumfungia msanii Zuhura Othman Soud (Zuchu) kufanya shughuli yoyote ya sanaa kwa Zanzibar kwa kipindi cha muda wa miezi sita kuanzia leo Machi 5, 2024,” amesema.
Amesema wanafanya hivyo kutokana na tabia yake kuimba nyimbo ambazo hazina maadili, hazifuati misingi na hazina afya njema kwa jamii ya Wazanzibari.
Pia, amesema licha ya msanii huyo kutokuwa na usajili Zanzibar lakini amekuwa akiendesha shughuli zake za sanaa bila kupata kibali.
Mbali na adhabu hiyo, pia msanii huyo ametakiwa kulipa faini ya Tsh milioni moja kwa Baraza la Sanaa na aandike barua ya kuomba radhi na kuthibitisha kwamba hatafanya kosa hilo ndani ya kipindi alichofungiwa.

Siku 10 nzito kwa Gamondi
Ajali: Ndege zagongana, wawili wafariki