Mshambuliaji wa Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Fiston Kalala Mayele ameendelea kusisitiza ushindi katika mchezo wa Mkondo wa Kwanza wa Ligi ya Mabingwa Barani Afrika dhidi ya Al Hilal ya Sudan.

Young Africans itaikaribisha klabu hiyo ya Sudan Jumamosi (Oktoba 08), Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam, huku mchezo wa pili ukitarajiwa kuchezwa Oktoba 14 mjini Khartoum.

Mayele amesema Wachezaji, Benchi la Ufundi na Viongozi wote wa Young Africans mpango wao mkuu ni kuhakikisha wanashinda mchezo wa nyumbani, akiamini utawapa mwanzo mzuri kabla ya mchezo wa Mkondo wa Pili.

“Iwe Mvua iwe Jua ushindi ni lazima katika mchezo wa nyumbani, kwa upande wa timu tumejipanga na tunaendelea kujiweka vizuri zaidi na tunaamini hilo litatimia kwani ni ndoto ya kila mchezaji kusonga mbele,”

Katika hatua nyingine Mshambuliaji huyo amekiri kuwafahamu Al Hilal kwa baadhi ya wachezaji na Kocha Mkuu Florent Ibenge aliyewahi kumfundisha alipokua AS Vita ya kwao DR Congo.

Amesema anafahamu namna Mashabiki wa Al Hilal wanavyoshanglia wanapokua nyumbani, hivyo inaendelea kumuaninisha kuwa hata watakapokua ugenini, watahakikisha wanapambana ili kufanikisha mpango wa kutinga hatua ya Makundi.

“Nilifuatilia mchezo wa Al Hilal waliocheza ugenini dhidi ya St George ya Ethiopia lakini pia nawafahamu baadhi ya wachezaji wao, wapo bora sana uwanjani, pia nje wana mashabiki wanaojua kushangilia kwa nguvu wakati wote, kwa haya hote ninaamini tukiwa kitu kimoja tutashinda na tutafanikiwa kusonga mbele.”

“Mashabiki kwetu ni Mchezaji wa 12, kila Shabiki siku hiyo natakiwa kuja uwanjani ili kuongeza hamasa kwetu sisi wachezaji, tunawaahidi tutapambana kwa moyo wote na tutawafurahisha kwa kushinda mchezo wa nyumbani kabla ya kwenda ugenini.” amesema Mayele.

Kabla ya kuivaa Al Hilal, Young Africans itacheza mchezo mmoja wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting, Uwanja wa Benjamin Mkapa Oktoba 03.

Ruvu Shooting yatamba kuvunja rekodi Ligi Kuu
Clatous Chama atajwa tena Simba SC