Askari anayejiita Faru John ameripoti Kituo Kikuu cha Polisi cha Kanda Maalumu ya Dar es Salaam alikohojiwa na kuruhusiwa kuondoka akaendelee na kazi.

Kuripoti kwa askari huyo kunatokana na agizo alilolitoa Kamanda wa kanda Maalum ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa kwa Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Peter Sima la kumpeleka kuhojiwa baada ya kutuhumiwa na wananchi wa Mbagala kuwa amekuwa akidai rushwa

Amesema kuwa Askari huyo ataendelea kufuatiliwa ili kubaini ukweli wa tuhuma zilizotolewa dhidi yake na endapo zitathibitishwa taarifa zitawasilishwa kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, nchini IGP Simon Sirro ili sheria ichukue mkondo wake.

“Kaimu kamanda wa polisi Mkoa wa Temeke alimleta huyu askari ambaye nimemuhoji na kumruhusu kuendelea na kazi wakati akiendelea kuchunguzwa ndani ya wiki moja,” amesema Kamanda Mambosasa.

Hata hivyo, Kamanda Mambosasa aliyekuwa akisikiliza kero za wananchi wa Mbagala Zakhem amesema kuwa Jeshi la Polisi haliwezi kuwa na askari anayejipa jina la mzaha, huku akiwakandamiza wananchi.

JPM atuma salamu za rambirambi ajali ya Uganda
Polisi yakamata waandamanaji nchini Uganda