Baada ya kutolewa katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, Kocha Msaidizi wa Azam FC, Vivier Bahati, amesema akili na nguvu zote sasa wanazihamishia katika michezo yao ya Ligi Kuu Tanzania Bara ukiwamo ule wa Oktoba 30, mwaka huu dhidi ya Young Africans.

Vivier amesema wamepokea matokeo hayo na sasa wanarejea nyumbani kujipanga kwa michezo iliyopo mbele yao ikiwamo ya Ligi Kuu na Kombe la Shirikisho ‘ASFC’.

Amesema mchezo ulikuwa wa ushindani mkubwa na baada ya kufungwa walilazimika kuanza kutafuta bao la kusawazisha, lakini hawakuwa na bahati, sasa nguvu wanazihamishia kwenye mchezo dhidi ya Young Africans.

“Ulikuwa mchezo mzuri tulijitahidi kupambana kwa ajili ya kupata matokeo, lakini tumeshindwa kufikia malengo sasa tunarudi nyumbani kupambana katika ligi, tunahitaji, kupambana na kufanya vizuri michezo yetu ya nyumbani,” amesema Vivier.

Amesema baada ya kushindwa kufikia malengo yao ya kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho, sasa wanarejea kuhakikisha wanapambana kutafuta matokeo mazuri katika michezo yao ya ligi wakianza na uliopo mbele yao dhidi ya Young Africans.

IS wahusika na ugaidi Uganda
Hati Fungani kuendesha Serikali za Mitaa