Watendaji wa Manispaa ya Kigamboni wamepongezwa kwa kufanya kazi kwa moyo wa kujituma ili kuweza kutimiza majukumu yao ya kila siku ambayo ni pamoja na kuwatumikia wananchi kwa kuwapatia huduma nzuri.

Hayo yamesemwa hii leo na Naibu Waziri wa Nchi  Ofisi ya Rais  Tamisemi, Selemani Jafo mara baada ya kufanya ziara ya kikazi  na kuzungumza na watumishi wa Manispaa hiyo mpya, ambapo amewapongeza kwa kuhakikisha wanatoa huduma bora na nzuri kwa wananchi.

Aidha, katika ziara hiyo, Jafo amefanikiwa kutembelea ujenzi wa mabweni, madarasa, maabara na vyoo katika shule ya sekondari ya Somangira ambapo serikali ilipeleka sh. milioni 259 ili kujengwa miundombinu hiyo na kufanya shule iwe na uwezo wa kupokea wanafunzi wa kidato cha tano waliochaguliwa kwa awamu ya pili.

Vile vile, Jafo ametembelea hospitali ya Vijibweni na kuwamwagia sifa watendaji wote wa hospitali hiyo kwa usimamizi mzuri kwa kuwa na mazingira ya usafi wa kuvutia.

Hata hivyo, Jafo amesema kuwa Serikali itatenga eneo Maalum kwa ajili ya duka Maalum la wagonjwa wa bima ya afya ili wagonjwa wote wa bima wasikose dawa wanapofika hospitalini kupata matibabu.

 

Video: Makonda apokea Pikipiki 10 za Askari wa usalama barabarani
Ziara ya Majaliwa nchini Cuba kuinufaisha Tanzania