Maafisa wa kijeshi wa Mali waliokasirishwa na mabadiliko ya Baraza la Mawaziri wanamshikilia Rais na Waziri Mkuu katika kambi ya jeshi, hatua inayolaaniwa vikali na jumuiya ya kimataifa na kutaka waachiliwe huru.

Taarifa ya pamoja iliyotolewa na Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika Magharibi(ECOWAS), Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, Umoja wa Ulaya, Marekani na Uingereza imetoa wito wa kuachiliwa huru mara moja kwa Rais Bah N’Daw na Waziri Mkuu Moctar Ouane, ambao wameshikiliwa katika kambi ya kijeshi.

Kukamatwa kwa viongozi hao wanaoongoza serikali ya mpito ambayo iliundwa kufuatia mapinduzi ya kijeshi mnamo mwezi Agosti, kumeongeza hofu ya kutokea mapinduzi mengine.

Viongozi hao walikamatwa baada ya kufanya mabadiliko ya baraza la mawaziri mapema jana ili kutuliza ukosoaji mkubwa uliokuwa ukiikabili serikali yao ya mpito.

Aidha Umoja wa Ulaya umesema uko tayari kuzingatia kuwachukulia hatua viongozi wa kisiasa na kijeshi ambao wanazuia kufanyika mabadiliko nchini Mali.

Rais wa Baraza la Ulaya, Charles Michel amesema, “Tunalaani kilichotokea Mali katika masaa machache yaliyopita, utekaji nyara wa Rais na Waziri Mkuu, na tunaunga mkono ujumbe uliotumwa na SADC na Umoja wa Afrika.”

Michel amesema kwa pamoja wanatoa wito wa kurudishwa kwa serikali ya mpito, na kwamba klichotokea ni kitu kikubwa na wako tayari kuzingatia kuchukua hatua zinazohitajika.

Neema yaishukia VPL
Azam Media kidume Ligi Kuu