Katika kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa kitu kimoja na kuondoa tofauti zao, Mkuu wa Wilaya ya Iringa Mjini, Richard Kasesela amewataka wananchi wa Wilaya ya Iringa Mjini kuacha tabia ya kuamini na kujihusisha na maswala ya imani za kishirikina pamoja na kujichukulia sheria mikononi.

Ameyasema hayo baada ya mwanananchi mmoja Mkazi wa Kijiji cha Mikong’wi Kata ya Kihologota Wilaya ya Iringa kuuawa na watu wasiojulikana kwa kukatwa kichwa na kutelekeza kiwiliwili chake.

“Kwanini watu wajichukulie sheria mikononi wakati Serikali, Jeshi la Polisi, Vyombo vya dola na taasisi mbalimbali za kutatua migogoro zipo, Serikali haiamini ushirikina hata kidogo na inasikitishwa kutokea kwa tukio baya kama hili ambalo linahusishwa na imani potofu za kishirikina”, Amesema Kasesela.

Aidha, Kasesela amesema kuwa wamepokea kwa masikitiko makubwa taarifa hiyo na amewataka wananchi wote kutojichukulia sheria mikononi kwa kuwa Serikali haiamini uchawi na ameliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi ili kubaini aliyehusika na tukio hilo.

Hata hivyo, amewaomba viongozi mbalimbali wa dini kutoa elimu ya mungu na kukemea maswala ya Imani potofu za kishirikina kwa kuwa yanapunguza nguvu kazi za wananchi.

Wananchi watakiwa kuweka kando itikadi zao
Wabunge wachachamaa, wapinga vikali matumizi ya Faru Fausta